Benki ya dunia imesema itaendelea kuwa mdau wa maendeleo wa Tanzania, ili kuisaidia nchi hiyo kuhimiza maendeleo na kuboresha huduma za jamii.
Uhakikisho huo umetolewa wakati baadhi ya vyombo vya habari vikitaja kuwa benki ya dunia inapanga kuifutia msaada Tanzania kutokana na uamuzi wa Rais John Magufuli wa kuzuia wanafunzi wanaopata ujauzito kuendelea na masomo mara baada ya kujifungua, na pia maboresho ya Sheria ya Takwimu yaliyopitishwa na Bunge la Tanzania Septemba 10 inayokandamiza uhuru wa kujieleza wa wananchi. Akiongea ikulu jijini Dar es salaam baada ya kukutana na makamu mkuu wa Benki ya Dunia barani Afrika Bw. Hafez Ghanem, Rais Magufuli wa Tanzania amethibitisha kuwa Benki hiyo imeridhia kutoa Dola milioni 300 za Kimarekani zikiwa ni sawa na shilingi bilioni 680.5 za Tanzania kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa kuongeza ubora wa elimu.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |