• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • China yatoa waraka kuhusu maendeleo ya mambo ya wanawake

    (GMT+08:00) 2019-09-19 18:29:28

    Ofisi ya habari ya baraza la serikali la China leo imetoa waraka kuhusu mambo ya wanawake, na kueleza mafanikio yaliyoipata China katika kuendeleza mambo ya wanawake katika miaka 70 iliyopita tangu kuanzishwa kwa Jamhuri ya Watu wa China.

    Waraka huo uitwao "Usawa, maendeleo na manufaa ya pamoja: mafanikio ya mambo ya wanawake katika miaka 70 iliyopita tangu kuanzishwa kwa Jamhuri ya Watu wa China umesema, katika miaka hiyo 70, mambo ya wanawake siku zote yamehusishwa na maendeleo ya shughuli za Chama cha Kikomunisti cha China CPC na taifa la China. Chini ya uongozi wa CPC, kizazi baada ya kizazi cha wanawake wametoa mchango muhimu kwa ajili ya ujenzi, mageuzi na maendeleo ya China. Kwa upande mwingine, wakati China iliposimama, kutajirika na kuwa na nguvu kubwa, hadhi ya wanawake pia imeinuka kwa kiasi kikubwa.

    Waraka huo unasema, tangu kufanyika kwa mkutano mkuu wa 18 wa Kamati Kuu ya CPC, kufuatia mawazo ya rais Xi Jinping ya kujenga ujamaa wenye umaalumu wa China katika zama mpya, mamilioni ya wanawake wa China wamekuwa na nia thabiti zaidi ya kuchagua njia ya ujamaa wenye umaalumu wa China ya kujiendeleza, kutekeleza haki, kushiriki kwenye maendeleo ya uchumi na jamii na kunufaika na mafanikio ya mageuzi kwa usawa na njia ya kisheria. Aidha, wadhifa wao wa kijamii na mchango wao kwa maendeleo ya taifa vimeongezeka, na pia upatikanaji wao wa manufaa, furaha na usalama umezidi kila siku. China imepata mafanikio makubwa yanayofuatiliwa na dunia nzima katika kuendeleza mambo ya wanawake.

    Waraka huo umesema, China siku zote inatilia maanani kuendeleza mambo ya wanawake na kusawazisha wadhifa wa wanawake na wanaume, na imekamilisha sheria za kulinda maslahi ya wanawake na kuimarisha mfumo wa shirikisho la wanawake.

    Waraka huo umesisitiza kuwa, mafanikio hayo yamepatikana kutokana na uongozi thabiti wa CPC na juhudi kubwa za mamilioni ya wanawake wa China kwa ajili ya ustawi wa taifa. Mchakato wa kupata mafanikio hayo ni mchakato wa kihistoria wa maendeleo ya pamoja ya mambo ya wanawake na mambo ya uchumi na jamii, kusawazisha wadhifa wa wanawake na wanaume na kuendeleza ustaarabu wa jamii, na pia ni mchakato wa wanawake wa China kushirikiana na wanawake wa dunia nzima kujenga dunia bora zaidi na kunufaika nayo kwa pamoja.

    Waraka huo umesema, maendeleo ya China yameingia katika zama mpya. Kuinua zaidi kiwango cha usawa kati ya wanawake na wanaume na maendeleo ya mambo ya wanawake kunakabiliwa na changamoto pamoja na fursa nzuri. China itafuata mawazo ya rais Xi Jinping ya kujenga ujamaa wenye umaalumu wa China, kushikilia kuboresha maisha ya wanawake inapoendeleza uchumi, kutosahau nia ya awali, kuendelea na juhudi za kuhimiza maendeleo ya wanawake kwa pande zote, na kuhamasisha wanawake kutoa mchango zaidi kwa ajili ya kutimiza "malengo mawili ya miaka 100" na ndoto ya China ya kustawisha tena taifa la China.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako