• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • China yamejenga mtandao mkubwa zaidi ya habari na mawasiliano duniani

    (GMT+08:00) 2019-09-20 19:09:29

    Waziri wa viwanda na habari wa China Bw. Miao Wei, leo hapa Beijing amesema katika muda miaka 70 iliyopita tangu Jamhuri ya Watu wa China ianzishwe, China imejenga mtandao mkubwa zaidi wa habari na mawasiliano duniani, na hivi sasa China inashika nafasi ya kwanza duniani kwa hataza za lazima za mtandao wa 5G, na mwakani itaanza rasmi kutoa huduma za mtandao huo katika sehemu mbalimbali nchini China.

    Kwenye mkutano na wanahabari ulioandaliwa na ofisi ya habari ya baraza la serikali la China, waziri wa viwanda na habari wa China Bw. Miao Wei ameeleza kuwa China imejenga mtandao mkubwa zaidi wa habari na mawasiliano duniani, akisema,

    "Idadi ya watu wa China inashika asilimia 20 ya idadi ya watu wote duniani, lakini kiasi cha vituo vya mtandao wa 4G kinashika nusu ya kiasi hicho cha dunia nzima, hivyo wachina wana huduma bora ya mawasiliano ya habari."

    Wakati huohuo, China imepunguza gharama z matumizi na kuongeza kasi ya mtandao. Tangu mwaka 2014, kasi ya mtandao wa Internet imeongezeka mara saba, lakini malipo ya wateja yamepungua kwa asilimia 90. Hivi sasa China inaharakisha maendeleo ya miundombinu ya kisasa ya habari na mawasiliano, ikiwemo 5G, mtandao wa mawasiliano ya kiviwanda na akili bandia. China imeshika nafasi ya kwanza duniani kwa idadi ya hataza za lazima za mtandao wa 5G. Hata hivyo imefungua mlango katika ushirikiano wa habari na mawasiliano. Bw. Miao anasema,

    "Likiwa soko linalostawi zaidi la sekta ya habari na mawasiliano, China inahamasisha uwekezaji binafsi kuingia sekta hiyo, na pia inapenda kunufaika na ustawi wa sekta hiyo pamoja na nchi nyingine, kwa kufungua mlango hatua kwa hatua. Aidha, tunaongeza ushirikiano na nchi zilizojiunga na 'Ukanda Mmoja, Njia Moja' katika sekta hiyo."

    Bw. Miao ameeleza kuwa hadi sasa katika soko la China kuna aina 11 za simu za mkononi zinazoweza kutumia mtandao wa 5G, na hadi mwakani, China itatoa rasmi huduma za 5G katika sehemu mbalimbali. Ameongeza kuwa licha ya simu za mkononi, teknolojia ya 5G itatumika katika mtandao wa mawasiliano ya kiviwanda, mtandao wa mawasiliano ya magari, na matibabu mtandaoni. Anasema,

    "Kwa mfano mtandao wa mawasiliano ya magari. Tumekubaliana na wizara ya mawasiliano ya barabara na wizara ya usalama kwamba, kuhimiza maendeleo ya mtandao wa mawasiliano ya magari kunahitaji kuzingatia magari pamoja na barabara. Lengo hili linaweza kutimizwa tu kwa teknolojia ya 5G."

    Kutokana na maendeleo ya teknolojia ya habari na mawasiliano, hadi kufikia mwishoni mwa mwaka jana, thamani ya uchumi wa kidata nchini China ilikuwa imezaidi dola trilioni 4.38 za kimarekani, ambayo ni theluthi moja ya pato la taifa GDP.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako