SOKA: Tanzania yaingia nusu-fainali kwenye michuano ya Cecafa ya U-20
2020-11-27 16:46:34| cri

Mabingwa watetezi Tanzania wamefuzu kushiriki nusu-fainali ya mashindano ya soka ya Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) kwa wachezaji wasiozidi umri wa miaka 20 baada ya kuinyeshea Somalia mvua ya magoli 8-1 mjini Arusha, jana Alhamisi. Ngorongoro Heroes, ambao walikung’uta 6-1 katika mechi ya Kundi A na ya kufungua mashindano haya mnamo Novemba 20, waliizamisha Somalia kupitia mabao ya Abdul Hamisi Suleiman dakika ya tatu, Ben Sarrkie (14), nahodha Kelvin Pius John (25, 33, 60), Kassim Haruna (47), Frank George (65) na Anuar Jabir (86). Somalia ilikuwa imesawazisha 1-1 kupitia mchezaji Sahal Muhamed dakika ya sita kabla ya kusambaratishwa kabisa. Leo Ijumaa itakuwa zamu ya Rising Stars ya Kenya dhidi ya Sudan katika mechi ya Kundi C. Stars ya kocha Stanley Okumbi ilianza kampeni yake kwa kuicharaza Ethiopia 3-0 Novemba 23. Sudan ilipigwa 3-2 na Ethiopia katika mechi yake ya kwanza hapo Novemba 25 kwa hivyo mechi ya Ijumaa inatarajiwa kuwa moto. Mshindi wa kundi C pia ataungana na Tanzania ambayo imeonyesha mapemamapema kuwa haitakubali taji litoke nchini humo.